Viongozi wa JKCI Hospital ya Dar Group wajengewa uwezo wa kudhibiti vihatarishi vya kiutendaji
Автор: MASTER VOICE TV
Загружено: 2025-10-24
Просмотров: 13
Viongozi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group wanahudhuria mafunzo ya kutambua na kudhibiti vihatarishi vinavyoweza kuathiri utendaji kazi wa hospitali hiyo, sambamba na kuimarisha utekelezaji wa mpango mkakati unaolenga kuboresha utoaji wa huduma bora kwa wananchi.
Akizungumza kuhusu mafunzo hayo ya siku tatu yanayofanyika jijini Dar es Salaam Mkurugenzi wa JKCI Hospitali ya Dar Group Dkt. Tulizo Shemu alisema mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada za taasisi hiyo kuhakikisha maendeleo ya kiutendaji hayaathiriwi na changamoto zinazoweza kuzuilika kupitia mipango thabiti.
Dkt. Shemu ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo na mtaalamu wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo alisema mafunzo hayo yataisaidia hospitali hiyo kuendelea kutoa huduma bora salama na endelevu kwa wananchi.
Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Fedha na Uhasibu wa hospitali hiyo CPA. Ashura Ally alisema uandaaji wa rejesta ya vihatarishi ni takwa la Wizara ya Afya ambapo kila taasisi ya umma inapaswa kuandaa rejesta hiyo ili kuimarisha utendaji wake.
Naye Mkuu wa Kitengo cha Ugavi na Ununuzi wa JKCI hospitali ya Dar Group Iddi Lemmah alisema mafunzo hayo ni nyenzo muhimu katika utekelezaji wa mpango mkakati wa miaka mitano wa taasisi hiyo kwani yamewasaidia kuelewa namna bora ya kuendesha taasisi kwa ufanisi.
JKCI Hospitali ya Dar Group inatoa huduma za matibabu ya moyo, kinywa na meno, matibabu ya magonjwa ya kuambukiza kama malaria, huduma za dharura, kliniki ya wanawake na wajawazito, kliniki ya macho, pua, masikio na koo, kliniki ya mfumo wa mkojo, matibabu ya magonjwa ya tumbo na ini, figo, huduma za baba, mama na mtoto (RCH), upasuaji mkubwa na mdogo, upimaji wa VVU na ushauri, fiziotherapia (mazoezi tiba), huduma za maabara na gari la wagonjwa.
#mastervoicetv #news
Доступные форматы для скачивания:
Скачать видео mp4
-
Информация по загрузке: